Tuesday, June 12, 2012

MBEYA UPDATE: AUNGUA NA MAJI YA MOTO, AFANYIWA MAOMBI HALI YAWA MBAYA

Mwanafunzi wa Kidato cha Pili(QT),Calvary Centre ya Mji mdogo wa Mbalizi,Wilaya ya Mbeya Vijijini,Mkoani Mbeya aliyefahamika kwa jina la  Sifa Brown(19),ameungua kwa maji ya moto mwezi mmoja uliopita lakini hakupelekwa Hospitalini kutokana na imani ya Kanisa analoabudu.
Hayo yamebainishwa na mtandao huu baada ya kufika katika Hospitali ya Ifisi Jijini Mbeya,ambapo binti huyo alifikishwa hospitalini hapo na Mkuu wa Kituo cha Polisi cha mji huo baada ya kupokea taarifa kwa wasamalia wema kuwa mtoto huyo kafichwa ndani akiendelea kufanyiwa maombi na waumini wa Kanisa la Uamusho wa Roho.

Kwa upande wake Binti huyo amejeruhiwa sehemu ya mikono,kiwiliwili na mgongoni,amesema kuwa anaishi  na Baba yake mkubwa Bwana Ambokile Abrahamu,ambaye pia ni muumini wa dhehebu hilo lililoko eneo la Simike jijini hapa.

Imeelezwa kuwa baba huyo alisema hakuna haja ya kwenda hospitalini hivyo yeye na mkewe waliendelea kumfanyia maombi binti huyo na hali kuzidi kuwa mbaya hali iliyopelekea mwili wake kuoza.

Muasisi wa kanisa hilo Mchungaji Nise Mwasomola alifariki Februari 12 mwaka 2010 na kanisa hilo linaongoza na kamati,ambapo Bwana Ambokile ni mmoja wa wanakamati na kitendo chake cha kumzuia binti huyo kupeleka hospitalini Jeshi la polisi lililazimika kuingilia kati.

Aidha binti huyo alifikishwa hospitalini hapo Juni 11 mwaka huu na hali yake kwa sasa anaendelea vema baada ya kuanza kupatiwa matibabu.

Hata hivyo Jeshi la polisi linamshikilia Bwana Ambokile Abraham na mkewe kwa kitendo hicho cha ukatili na ukiukaji wa haki za binadamu kwa kisingizio cha imani ya kidini.

Kwa uapande wake msemaji wa Hospitali ya Ifisi Bwana Goodluck Lession,amesema wanafanya kila jitihada ili binti huyo apone ingawa alicheleweshwa sana na kusikitishwa na kitendo kilichofanywa kwa binti huyo.

Mwenyekiti wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la polisi Bi Mary Gumbo,amewataka wananchi kufichua vitendo viovu vinavyofanywa na baadhi ya wanawake kwa watoto wanaowalea.

Kamanda wa Jeshi la polisi Diwani Athuman,amethibitisha kutokea kwa tukio hili na kwamba watuhumiwa watafikishwa mahakamani pindi upelelezi utakapo kamilika.

Mkoa wa Mbeya ni moja ya mikoa yenye madhehebu mengi,lakini mengi yamekuwa hayazingatii maadili ya dini.

No comments:

Post a Comment