Monday, June 4, 2012

TANZANIA POLITICAL NEWS: JK ATAKIWA KUTOA TAMKO KUHUSU USHOGA


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemtaka Rais Jakaya Kikwete atoe tamko na msimamo wa Tanzania kuhusu hatua ya Rais Barack Obama wa Marekani kuidhinisha sheria ya ushoga nchini mwake.
Akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika juzi kwenye Kata za Mnavira na Mchauru, Jimbo la Lulindi, Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CHADEMA, John Mnyika alisema ukimya wa Rais Kikwete hauleti picha nzuri katika suala hilo linalopingwa na dini zote.

Kauli hiyo ya Mnyika ilifuatia swali aliloulizwa na Katibu wa Chama cha Wananchi (CUF), Kijiji cha Rivango, Keneth Khamis aliyetaka kujua ukweli kuhusu taarifa zilizowasilishwa kwao, zikieleza kuwa CHADEMA inaunga mkono ushoga na usagaji, kutokana na kuwa na uhusiano na ushirikiano na chama cha Conservatives cha Uingereza.

Amesema hizo ni propaganda zilizopangwa na CCM ili CHADEMA kisikubalike katika jamii, na kusema kauli iliyowahi kutolewa na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye ikiihusisha CHADEMA na kuunga mkono ushoga ni ya unafiki. Amesema baada ya Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron kuukubali ushoga na usagaji na kutaka iwe sehemu ya masharti kwa misaada inayotolewa na nchi za Magharibi, CHADEMA ilipinga na kuweka wazi kwamba haiungi mkono ‘uchafu’ huo. Mnyika amesema kutokana na Rais Kikwete kwenda Marekani kwa lengo la kutafuta misaada, kuna dalili ya kuwepo uwezekano wa taifa hilo kupenyeza ajenda ya ushoga na ikakubaliwa na serikali kama ilivyotokea kwa Malawi.

No comments:

Post a Comment